Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024, Ndg. Godfrey Eliakimu Mnzava ameweka jiwe la msingi kwenye mradi wa ujenzi wa jengo la maktaba, unaoendelea ndani ya Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi.



Tukio hilo limeshuhudiwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda, Katibu Mkuu wa wizara hiyo Prof. Carolyne Nombo, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi Mhe. Anne Makinda, Viongozi mbalimbali pamoja na Watumishi.



Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge Kifaifa, Makamu Mkuu wa Chuo Prof. Alfred Sife Mradi amesema kuwa, mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi “Group Six International Limited” kwa fedha za maendeleo kutoka Serikali Kuu kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na ukikamilika utakuwa na uwezo wa kuchukua wasomaji 2,500 kwa wakati mmoja, hivyo kuboresha mahitaji ya kufundishia na kujifunzia.



Hotuba hiyo imeainisha kuwa, kukamilika kwa mradi husika kutapunguza msongamano wa watumiaji wa huduma za maktaba kwenye jengo la zamani, kuongeza idadi ya ofisi kwa ajili ya watumishi wa Chuo, kuongeza idadi ya kumbi za mikutano, kuwavutia na kuongeza idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa pamoja na kusaidia wakazi wa Mkoa Kilimanjaro kupata huduma bora na za kisasa za Maktaba.



Prof. Sife amebainisha kuwa, Gharama za mradi ni shilingi 8,967,040,710.00 (Billioni nane nukta tisa) ikijumlisha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ambapo mpaka sasa umefikia 40% ya ujenzi wote.



Mradi wa ujenzi wa maktaba ulianza rasmi tarehe 12 Septemba, 2022 na unatarajiwa kukamilika tarehe 11 Septemba, 2024.

Jengo hilo litakuwa na ghorofa nne na ukubwa wa mita za mraba 9,732.45 ambalo litakuwa na mjumuiko wa ofisi za watumishi 7, sehemu za kusomea 27, vyumba vya kompyuta 2, vyumba vya semina 3, kumbi za mikutano 2 pamoja na vyumba vya majadiliano 3.