Serikali imesema Mwongozo wa Kitaifa wa Ulinganifu wa Sifa na Tuzo za Kitaaluma (Tanzania Qualifications Framework) unalenga kuainisha sifa za Kitaaluma pamoja na kuwezesha Watanzania kufanya kazi nchini na nje ya nchi.
Akifungua Mkutano wa Wadau wa Elimu wa kujadili Rasimu ya Mwongozo wa Taifa wa Ulinganifu wa Sifa na Tuzo za Kitaaluma Jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Eliamani Sedoyeka amesema Mwongozo huo utaweza kuwianisha Viwango, Maarifa, Ujuzi na Umahiri unaohitajika kwenye mfumo wa elimu na mafunzo.
Profesa Sedoyeka ameongeza kuwa uandaaji wa Mwongozo huo umefuata mfumo wa SADC Qualifikacations Framework na kuzingatia matakwa ya soko la ajira la pamoja la Afrika Mashariki.
Naye Mkurugenzi wa Idara ya Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Dkt. Noel Mbonde amesema wadau waliopata nafasi ya kutoa maoni katika Rasimu hiyo watafanya kazi hiyo kwa uaminifu na umakini ili kuwezesha nchi kupata Mwongozo utakaowezesha kutambulika duniani na Watanzania kufanya kazi ndani na nje ya nchi.
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe ambae pia ni Mwenyekiti wa Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu Nchini, Profesa Lughano Kusiluka amesema wanafarijika na hatua hiyo kubwa na muhimu itakayotoa mwongozo wa aina ya Mafunzo, sifa na ujuzi unaohitajika katika soko na wako tayari kuitolea maoni kwa manufaa ya Taifa .