BENKI YA DUNIA YAMPONGEZA SAMIA KWA KUWAREJESHA SHULE WANAFUNZI WAJAWAZITO

Published on Tuesday 12 July, 2022 07:45:05

Makamu wa Rais wa  Benki ya Dunia anayesimamia Kanda  ya Kusini mwa Afrika, Bi Victoria Kwakwa Julai 11, 2022 ametembelea shule ya Sekondari Turiani Jijini Dar es  Salaam ili kujionea maendeleo ya Programu ya SEQUIP ambayo sehemu ya utekelezaji wake ni mpango wa kuwarudisha shuleni watoto  walioacha masomo kutokana na sababu mbalimbali  ili waweze kuendelea na masomo yao.

Akizungumza shuleni hapo akiwa ameongozana na mwenyeji wake Waziri  wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof Adolf Mkenda  kiongozi huyo amesema amefurahi kupata nafasi ya kutembelea shule hiyo na kuona mabadiliko makubwa yaliyofanywa na Serikali ya  Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuendeleza sekta ya elimu ili kuzalisha nguvu kazi. 

Amepongeza kwa hatua aliyochukuliwa na Mhe. Rais ya kuwapa tena fursa wanafunzi ambao walikatisha masomo kutokana na sababu mbalimbali ili wapate elimu ambayo itawawezesha kujiletea maendeleo kwao wenyewe na familia zao pamoja  na kuchangia katika uchumi wa Taifa.

Kwakwa amesema Benki ya Dunia itaendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha watoto wa Kitanzania wanapata elimu bora kwenye miundombinu na mazingira salama ya kujifunzia pamoja na kuondoa changamoto zinazokwamisha mchakato wa ujifunzaji.

Akizungumza katika ziara hiyo Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof Adolf Mkenda amesema Serikali ina mkakati mkubwa wa kuhakikisha watoto wote walioacha shule kwa sababu mbalimbali ikiwemo ujauzito wanarudi na kuendelea na masomo yao.

Kiongozi huyo amesema benki hiyo imefadhili programu ya SEQUIP ambayo imewezesha kuwarudisha shuleni wanafunzi wapatao 3,333 ambao waliacha shule kutokana na sababu mbalimbali ambapo takribani wanafunzi 900 wamerudi katika mfumo rasmi na wengine katika mfumo wa elimu mbadala.

Ameongeza kuwa Makamu wa Rais huyo amefika katika shule hiyo ili kuona na kuongea na mabinti waliorudi shule kupitia programu ya SEQUIP inayofadhiliwa wa Benki ya Dunia ili kuangalia maendeleo yao.

Read 875 times

Contact

  • Name:    Permanent Secretary
  • Address: Government City
  • Mtumba Area - Afya Street
  •               P.O.Box 10
  •               40479 Dodoma
  • Tel:        +255 26 216 0270               
  •                +255 737 962 965
  • Email:    info@moe.go.tz
  • Zonal SQA Offices Contacts
Top